Matata Matatuni

“Ah! Bwana we! Unataka nikae vipi?” Nilimuuliza utingo aliyekuwa anajaribu kuweka mzigo fulani chini ya miguu yangu.

“Inua miguu, jamani,” alijibu huku akiishiwa na subira.

“Siinui ng’o!” Nilijibu kwa fadhaa.

“Aaah! Inua miguu bwana! Kwani unadhani wewe ndiye nani?”

“Sitainua. Utaninyima raha hadi lini wewe? Kwani sijalipia nafasi yangu kwenye matatu hii? Umenifinya vya kutosha kwa kujaza matatu kupindukia, na sasa unataka niinue miguu pia? Haiwezekani!”

“Acha ukorifi, jamaa. Hii ni matatu sio gari binafsi. Kama unataka starehe jinunulie gari.”

“Ni haki yangu kustarehe kwenye matatu nikichagua kusafiri kwa matatu. Kwani umenibeba bila malipo? Si nimelipia nafasi hii? Kama nimeilipia, nina haki ya kustarehe.”

“Eih! Inua miguu wewe! Kwani tutaishi hapa?” Abiria mmoja alibisha. Wengine pia walikuwa wameanza kunung’unika.

“Siwezi!” Nilijibu kwa ugombezi. “Watu kama nyinyi ndio mnasababisha tunakanyagwa kiasi hiki. Sasa ona tulivyofinyana. Matatu inafaa kubeba watu kumi na wanne lakini humu ndani tuko zaidi ya ishirini. Na nauli tumelipa, tena kiwango cha juu sana. Mnakubalije kutendewa hivi?”